Sunday, July 8, 2012

NINI HATMA YA MGOGORO WA WAPALESTINA NA WAYAHUDI?

NINI HATMA YA MGOGORO WA WAPALESTINA NA WAYAHUDI?
  • NANI ANAPASWA KUWA MMILIKI HALALI WA NCHI HIYO?
  • JUHUDI ZA USULUHISHI ZITAFANIKIWA?
 
NA JOSEPH MWAMBIJE
 
Mgogoro uliopo kati ya Wayahudi(Waisraeli) na Wapalestina umeigawanya dunia ambapo wapo wanaoamini kuwa Wayahudi ndio wanaopaswa kuwa wamiliki halali wa Nchi ya Israeli na wapo wanaoamini kwamba Wapalestina ndio wanaopaswa kuikalia Nchi hiyo kama Nchi yao .
 
   Kwa watu wengine Wayahudi wanaonekana ni watu wakatili wanaoikalia Nchi hiyo kimabavu huku wakiwanyanyasa Wapalestina.
 
    Wakati baadhi ya watu wanadai Wayahudi ndio  wenye Nchi hiyo na Wapalestina wanaonekana ni Magaidi na watu  wakorofi wanaowanyanayasa Wapalestina.Baadhi  ya Wasomi na wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanaona kwamba Wapalestina wanatendewa visivyo.
 
Baadhi ya Waislamu wao  wanalichukulia suala la kunyanyaswa Wapalestina kuwa ni la mgogoro wa kidini na kwamba Wapalestina wananyanyaswa kwasababu ya Uislamu wao.
 
    Kimsingi mgogoro wa Wayahudi na Wapalestina umegawanyika kidini na kisiasa. Waisraeli ndio wenye Nchi kidini lakini kisiasa Wayahudi au Waisraeli ni wakoloni wanaoikalia Nchi ya Wapalestina kimabavu.
 
    Imeshindwa kueleweka kwamba mgogoro wa Waisraeli na Wapalestina utatatuliwa kwa njia gani kwani Mataifa haya mawili yote yanaonekana  kufanya harakati kwa njia zinazotafsiriwa kuwa za kigaidi.
 
    Wengine wamekuwa wakiilaumu Marekani kwamba inawapendelea Waisraeli kitu ambacho mimi naona si kweli kulingana na mgogoro wenyewe, ila ninachokiamini hapa ni ugumu wa mgogoro wenyewe.
 
    Yameandikwa mengi kuhusiana na mgogoro huo na kila mmoja ametoa maoni yake namna ya kutatua mgogoro huo. Imeundwa mikataba mingi ili kuleta amani katika Nchi hiyo na eneo la Mashariki ya Kati.
 
    Wapalestina wamekuwa wakidai kunyanyaswa na Waisraeli kwa kupigwa na kutemewa mate usoni mbele ya watoto wao kitu kinachowafanya wakate tama na kujitoa muhanga kwa kujiua wenyewe ili mradi wameuwa Wayahudi kadhaa.
 
    Mbinu hiyo ya Wapalestina sijui walifundishwa na nani kwani inaonekana ni ya kujidhalilisha zaidi kuliko kutetea maslahi yao .
 
     Pengine tuyaangalie madai ya Wapalestina yanayowafanya wapambane na Waisraeli kufa na kupona. Kimsingi Wapalestina wanapigania haki ya kuwepo Taifa kamili la Kipalestina, Mji wa Jerusalemu  ambao ndio wanadai Mji Mkuu wa Nchi yao na kurudi kwa Wapalestina zaidi ya Milioni 5 ambao ni wakimbizi katika Nchi mbalimbali Duniani ambapo kwa sheria za Israeli hawaruhusiwi kurudi Palestina bila kibali maalumu.
 
    Watu wengi wamekuwa wakijiuliza nini hatma ya mgogoro wa Waisraeli na Wapalestina. Kila mmoja anatoa majibu yake jinsi anavyoufahamu mgogoro huo. Hata hivyo majibu ya msingi ya namna ya kutatua mgogoro huo yanakosekana.
 
    Kufuatia mgogoro huo maswali ya  msingi yamekuwa yakijitokeza na watu wengi wamekuwa wakijiuliza maswali mengi bila majibu,baadhi ya maswali hayo ni kwa nini Waisraeli na Wapalestina wanashindwa kuelewana, nani atamaliza mgogoro wa Mataifa hayo na Je mgogoro baina ya Mataifa hayo utakwisha na je Wapalestina wataweza kujikwamua kwenye makucha ya Waisraeli?.
 
    Mgogoro wa Waisraeli na Wapalestina una mlolongo mrefu sana uliochanganyika na udini ndani yake na ambao unawachanganya watu wengi na kuwaachia maswali mengi.
 
    Kama nilivyosema awali kwamba kuna Mikataba mingi iliundwa ili kujaribu kuleta amani katika Nchi hiyo ya Palestina huko Mashariki ya Kati. Moja ya mikataba iliyoundwa na inayokumbukwa ni Mkataba wa Oslo ambao ulisainiwa katika Hoteli ya Plaza Mjini Oslo Norway Septemba 13, 1993.
 
    Mkataba huo ulipingwa na baadhi ya wasomi wa kiarabu wakidai una kasoro nyingi na baadhi ya wasomi hao walidai kuwa mkataba huo uliokuwa na vifungu 17 na kurasa 14 za ufafanuzi ulikuwa na mapungufu mengi.
 
    Wasomi hao walisema upungufu wa kwanza katika mkataba huo ni kuwaondolea Wapalestina hadhi ya kuwa Taifa kamili na kuishia kuwapa uwezo wa kuwa na mamlaka ya ndani (Internal Palestinian Authority ).
 
    Upungufu wa pili wasomi hao walisema mazungumzo ya mkataba huo hayakugusia lolote kuhusu hatma ya Mji wa Jerualem ambapo Wapalestina wamekuwa wakiupigania sambamba na Taifa lao.
 
     Wapalestina wanadai Jerusalem ndio makao yao makuu na kwamba utakuwa Mji Mkuu pindi watakapounda Taifa lao. Wasomi hao walisema mkataba utakaokwepa kuzungumzia hatma ya Jerusalem watakwepa kuuzungumzia.
 
    Kimsingi mkataba huo wa Oslo haukuweza kutatua matatizo baina ya Waisraeli na Wapalestina zaidi ya kuongezea matatizo na lawama nyingi kumwangukia aliyekuwa kiongozi wa Wapalestina wa wakati huo Marehemu Yasser Arafat kwa kuukubali mkataba huo.
 
    Manyanyaso ya Waisraeli dhidi ya Wapalestina yalipelekea kuundwa kwa chama cha Ukombozi wa wapalestina PLO, kilichoongozwa na Marehemu Ysser Arafat. Karibu Nchi zote zilizokuwa zikitawaliwa hapa duniani zimejikomboa kutoka kwenye makucha ya wakoloni na kujitawala, swali ni kwamba ni lini Wapalestina watapata Uhuru  wao?.
 
    Je watumie njia gani kuwatimua Waisraeli kwenye Nchi wanayodai ni ya kwao, je watumie mtutu wa Bunduki ambao ulishindwa kwenye vita ya Mwaka 1967 iliyojulikana kama vita ya siku saba, pale Waarabu walipoungana ili kuwaondoa Waisraeli katika Nchi hiyo ya Mashariki ya Kati. Je watumie mdomo kuwabembeleza Waisraeli kuondoka Nchini humo na kama wakiondoka watakwenda kuishi wapi? Hayo ni maswali magumu kujibiwa.
 
    
    Kisiasa Waisraeli wanaonekana ni walowezi na wakoloni ambao wanaikalia Nchi isiyo yao kimabavu  na  wanaonekana ni watu wakatili na wasio na huruma kwa wenyeji wao Wapalestina. Wanaonekana kama wakaburu wa Afrika ya Kusini katika miaka ya nyuma au Wareno katika Nchi ya Msumbiji katika enzi za ukoloni. Lakini la kujiuliza ni kwamba hawa ni wakoloni wa aina gani wanaotaka kukaa kwenye Nchi ya wenzao milele licha ya kelele zinazoambatana na machozi ya mamba za baadhi ya Mataifa makubwa ya Ulaya.
 
    Baadhi ya wasomi na wachunguzi wa mambo ya kisiasa wanasema Wapalestina ndio wanaopaswa kuikalia kihalali Nchi hiyo ya Palestina na kwamba Wayahudi walifika tu hapo na kuikalia Nchi hiyo.
 
    Hebu tuangalie kidini Taifa hili la Israeli kwa kuangalia Kitabu Kitakatifu cha Biblia na baadhi ya vitabu vya dini. Kimsingi Taifa hili lenye nguvu za kijeshi linaanzia kwa mtu mmoja anayeitwa Abramu ambaye baadaye alibarikiwa na Mungu na kuitwa Ibrahimu.
 
    Baadhi ya maandiko toka kwenye Biblia yanasema mimi agano langu nimelifanya nawe, nawe utakuwa Baba wa Mataifa mengi wala jina lako hutaitwa tena Abramu, lakini jina lako litakuwa Ibrahimu kwani nimekuweka uwe Baba wa Mataifa mengi.
 
    Nitakufanya uwe na uzao mwingi sana , nami nitakufanya kuwa Mataifa, na wafalme watatoka kwako. Agano langu nitalifanya imara kati ya mimi na wewe na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa Agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baba yako. Nami nitakupa wewe uzao wako baada yako Nchi hii unayoikaa ugeni, nchi yote ya Kaanani kuwa milki yako ya milele. (Mwanzo 17:4-7).
 
    Mungu alimtokea Ibrahimu wakati akiwa na miaka 100 na mkewe Sarai akiwa na miaka 90 na kusema, Sarai mkeo hutamwita jina lake Sarai, kwa kuwa jina lake ataitwa Sara. Nami nitambariki na tena nitakupa mwana kwake, naam nitambariki, naye atakuwa mama wa mataifa na wafalme wa kabila watatoka kwake. (Mwanzo 17:15-16).
 
    Baada ya kuambiwa maneno hayo na Mungu Ibrahimu na Sara hawakuamini kwani walikuwa wazee na miaka yote waliishi bila kupata mtoto ambapo Sara alikuwa tasa. Licha ya mashaka hayo waliyokuwa nayo Ibrahimu na Sara lakini Mungu aliwasisitiza kwamba watapata mtoto ambaye watamwita Isaka.
 
    Kwa Mungu hakuna linaloshindikana baada ya muda ule uliotamkwa na Mungu kwamba Sara angepata mimba akapata mimba na kumzalia Ibrahimu mtoto wa kiume katika uzee wake. Ibrahimu akamwita mtoto huyo Isaka kama Mungu alivyosema (Mwanzo 21:1-3).
 
    Kimsingi Ibrahimu ambaye Baba yake aliitwa Tera ndio Msingi mkubwa wa Taifa hili. Isaka alizaa watoto wawili mapacha, akawaita Esau ambaye alikuwa mkubwa yaani Kulwa na mdogo aliitwa Yakobo, yaani Doto. Kama ilivyo kwa mama yake pia mke wa Isaka aliyeitwa Rebeka alikuwa Tasa, watoto hao aliwapata baada ya kumwomba Mungu (Mwanzo 25:21,24:26).Esau alikuwa mwindaji hodari wakati Yakobo alitulia nyumbani. Isaka alimpenda Esau lakini Rebeka mkewe alimpenda Yakobo.
 
    Wakati Isaka alipokuwa Mzee akikaribia kufa akataka kumbariki mwanaye mkubwa Esau kutokana na uzee Isaka alikuwa amepofuka macho. Ilikuwa desturi za wakati ule Baba kumbariki mwanaye wa kwanza kabla ya kufa.
 
     Isaka akamwita mwanaye wa kwanza, Esau na kumweleza kwamba yeye ameshakuwa mzee hivyo  anataka kumbariki kabla hajafa, akamwambia amfanyie chakula kitamu kabla hajambariki kama ilivyokuwa desturi ya wakati huo. Esau alipoambiwa hayo akaenda nyikani kuwinda ili amtengenezee Baba yake nyama kama alivyomuagiza.
 
    Wakati Isaka akizungumza na Esau ndani Rebeka alisikia na akamwita Yakobo na kumwambia nimemsikia baba yako akimwambia Esau akatafute mawindo amfanyie chakula ili apate kumbariki.
 
     Rebeka akamwambia Yakobo akamletee mbuzi wawili ili akamtengenezee na akampe baba yake ili apate kumbariki. Kulikuwa na mabishano kati ya Yakobo na Mama yake ambapo Yakobo akamwambia Mama yake kwamba Esau ni mtu mwenye malaika (Vinyoleo) kifuani na mikononi hivyo baba yake atakapompapasa na kugundua yeye si Esau atamlaani hivyo laana haiwezi kuwa mbaraka, lakini mama yake akamwambia laana hiyo iwe juu yake.
 
     Yakobo akafanya kama mama yake alivyomuagiza akamletea mbuzi wawili. Mama yake akawatengeneza Mbuzi hao na kuchukua mavazi ya Esau mwanawe mkubwa na kumpa Yakobo ayavae, wakati hayo yote yakifanyika Esau alienda porini kuwinda.
 
     Mama yake Yakobo akachukua ngozi ya Mbuzi na kumvika Yakobo mikononi na kumpa nyama ya Mbuzi iliyotengenezwa vizuri na mikate akampe Baba yake. Yakobo alipofika mbele ya Baba yake akasema nimefika Baba na nimefanya kama ulivyoniagiza.
 
     Yakobo akamwambia baba yake inuka ule ili unibariki. Baba yake alipomuuliza wewe ni nani Yakobo akasema mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza. Isaka Baba yake akamuuliza imekuwaje umefanya haraka namna hii, Yakobo akajibu Bwana Mungu wako amenifanikisha.
 
     Yakobo akamwambia Baba yake inuka unipapase, naye alipompapasa mikononi akasema mikono ni ya Esau lakini Sauti ni ya Yakobo maana hakumtambua. Baada ya kula Isaka akambariki mwanaye.
 
 
 
 
Yakobo alipotoka tu Esau naye akawa anaingia kutoka katika mawindo yake. Esau akamwambia Baba yake ondoka ule mawindo yangu ili unibariki. Isaya akamuuliza U’ nani wewe, akamjibu mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza. Isaka akatetemeka na kushangaa na kuhoji ni nani aliyekuja na mawindo akaniletea, nami nimeshakula kabla hujaja wewe, nikambariki, naam naye atabarikiwa.
 
    Baada ya kuambiwa maneno hayo Esau akalia kilio kikuu akisema nibariki na mimi, Isaka akamjibu ndugu yako amekuja kwa hila na kuchukua mbaraka wako. Baada ya hayo Esau akamchukia sana Yakobo na akapanga kumuua.
 
    Rebeka Mama yao Esau na Yakobo aliposikia kwamba Esau anapanga kumuua Yakobo alimwambia Yakobo mwanae akimbilie Harani kwa Lutu ndugu yake. Akamwambia akae huko hadi hasira ya ndugu yake itakapopungua na atakaposahau aliyotendewa. (Mwanzo 27:1-46) Kimsingi alikokimbilia Yakobo ni sehemu za Mashariki ya Kati ya leo.
 
    Yakobo akiwa huko katika Nchi ya ugeni malaika wa Mungu alimtokea na kuongea naye na kumuuliza jina lake anaitwa nani. Akamjibu kuwa anaitwa Yakobo. Malaika akamwambia hutaitwa tena Yakobo bali utaitwa Israeli (Mwanzo 32:27-28).
 
    Kimsingi Taifa la Israeli ambalo linasuguana na Wapalestina huko Mashariki ya Kati linaanzia hapo. Ni habari za uhakika kwamba Mungu alilibariki Taifa hilo katika msingi wa kidini na si wa kisiasa na asili ya dini ya kikristo ni kutoka Taifa hilo ambalo Biblia imelitaja kama Taifa teule la Mungu.
 
    Mungu aliliteua Taifa hilo kama chanzo cha kufikisha Injili yake kwa mataifa mengine, ndio maana Wayahudi walikuwa hawachangamani na Mataifa mengine hadi alipokuja Yesu kuondoa utengano huo na kuwaambia Wayahudi wasiwaite Najisi wale walioumbwa na Mungu.
 
    Uteule wa Wayahudi kidini kama Taifa teule la Mungu ulikoma baada ya kumkataa Yesu na kumsulubisha msalabani na kumuua Mtume wake aliyeitwa Stephano. Kuanzia hapo sasa Injili iliwageukia Mataifa, yaani watu wengine wasio Wakristo na katika Dunia yote na ndio maana Wakristo wengine wanajiita Waisraeli wa Kiroho.
 
    Lakini licha ya Wayahudi kumkataa Yesu hawakunyang`anywa mibaraka waliyopewa pamoja na nguvu za kijeshi walizopewa. Istoria ya awali inaonyesha kwamba mapigano kati ya waisraeli na Waarabu ni ya muda mrefu, pengine tunaweza kuyaita mapigano yao kuwa ya Jadi. Kwa mujibu wa Kitabu Kitakatifu cha Biblia, mapambano hayo yamekuwa yakitegemeana ambapo mara nyingine Waisraeli walikuwa wakipigwa na mara nyingine Wapalestina walikuwa wakipigwa.
 
    Taifa hilo Teule limepitia katika mlolongo mrefu sana wa kutekwa na Mataifa mengine kama adhabu iliyotolewa na Mungu kuliadhibu Taifa hilo . Waisraeli walikuwa watu wa kuhama hama wakitafuta mahali panapowafaa kwa kuishi.
 
    Katika kulielezea Taifa la Israeli hatuwezi kuacha kuelezea habari za mtu mmoja aitwae Yusufu. Huyu alikuwa mtoto wa mwisho wa Yakobo. Alikuwa kijana mwenye miaka 17 kwa wakati huo, pia alikuwa mzuri wa sura (Handsome). Katika hatua za awali alionekana kwamba angekuwa mtu  mkubwa kwa nyadhifa baadaye kwani alikuwa akiota ndoto za ajabu ajabu ambazo ziliashiria hilo .
 
    Baba yake alimpenda kuliko watoto wake wote. Alimshonea vazi zuri. Baada ya kushonewa vazi hilo wivu uliibuka toka kwa ndugu zake. Siku moja Baba yake alimtuma Yusufu kuwapelekea chakula ndugu zake machungani walikokuwa wakichunga. Walipomwona kwa mbali akija wakasemezana tazama mwota ndoto yule anakuja, tumuue.
 
    Kaka yake aliyeitwa Reuben akasema tusimuue bali tumtupe humu kwenye shimo. Wakachukua chakula wakamvua kanzu yake na kumtupa kwenye shimo. Wakati wakila chakula waarabu wakapita wakielekea Misri ndipo ndugu zake wakashauriana na kumuuza kwa Waarabu.
 
    Ndugu za Yusufu wakamuuza Yusufu kwa vipande 20 vya fedha. Waarabu wakamchukua Yusufu hadi Misri. Ndugu hao wa Yusufu wakachinja Kondoo na kuirarua kanzu ya Yusufu na kumwagia damu ya Kondoo. Waliporudi wakamwambia Baba yao kwamba mnyama mkali amemla Yusufu. (Mwanzo 37:5-36). 
    Yusufu alipopelekwa Misri alipandishwa cheo na kuwa Waziri Mkuu kutokana na kipaji alichokuwanacho cha kutafsiri ndoto ambapo alitafsiri ndoto aliyoota Farao juu ya miaka 7 ya mavuno na miaka 7 ya njaa. (Mwanzo 40:1-57).
 
    Kwa mujibu wa Kitabu Kitakatifu cha Biblia ni kwamba baada ya miaka 7 ya mavuno kupita kulikuwa na njaa katika Dunia yote isipokuwa Nchi ya Misri ambako walihifadhi chakula wakati ule wa miaka 7 ya Neema(mavuno).
 
    Huo ndio ulikuwa mwanzo wa Taifa la Israeli kwenda utumwani Misri kwani kulipokuwa na njaa katika Nchi ya Israeli Yakobo na wanawe walihamia Misri ambako waliishi kwa raha mustarehe hadi alipokuja Farao asiyemtambua Yusufu (Mwanzo 46:8-27).
 
    Waisraeli wakaanza kuzaana kwa kasi kuwashinda Wamisri wakati wana wa Israeli wakiendelea kuzaana akainuka Farao mpya asiyemfahamu Yusufu na kuwaambia Wamisri angalieni Waisraeli wengi tena wana nguvu kuliko sisi.
 
    Farao akasema tunapaswa kutumia akili kwani ikitokea vita wanaweza kuungana na maadui zetu na kutupiga, Basi Wamisri wakakubaliana kuwawekea Waisraeli wasimamizi ili wawatese. Kadri walivyowatesa ndivyo Waisraeli walizidi kuongezeka. Waisraeli wakafanyishwa kazi kama watumwa ambapo walifanya kazi za mashambani, walijenga mapiramidi ambamo wafalme wa Misri walizikwa.
 
    Alipoona Waisraeli wanazidi kuongezeka Mfalme alipitisha Amri kwamba akizaliwa mtoto Muizraeli wa kiume auawe na kama wa kike asiuawe. Amri hii walipewa wakunga.
 
    Wakati Waisraeli wakiteseka mikononi mwa Wamisri Mungu akamuandaa mkombozi wa kuwakomboa Waisraeli katika makucha ya Farao. Mkombozi huyo si mwingine bali ni Musa aliyezaliwa katika Nchi ya Misri.Musa alipozaliwa alifichwa kando ya    mto ili asiuawe na binti wa Farao wakati kienda kuoga alimuokota na akatatafuta msichana wa kiyahudi kwa ajili ya kumlea. (Kutoka 1:1-22, 2:1-25).
 
    Mungu alimwandaa Musa kwa ajili ya kuwakomboa Waisraeli utumwani Misri, Musa aliandaliwa kukabiliana na Farao Mfalme wa Misri ili aweze kuwaachia Waisraeli.
 
    Musa alienda kuzungumza na Farao ili awaruhusu Waisraeli waweze kuondoka Misri kuelekea kwenye Nchi ya ahadi ambayo Mungu aliwaahidi.
 
    Farao alikuwa mgumu kuwaruhusu Waisraeli waondoke Misri hadi pale Musa alipofanya  miujiza mingi ili Farao aweze kuamini kwamba Musa ametumwa na Mungu. Muujiza wa mwisho uliomfanya Farao aamini kwamba Musa ametumwa na Mungu ni ule wa kuuawa kwa mzaliwa wa kwanza wa Misri ambapo waliuawa wanyama hadi wanadamu. (Kutoka 12:29-31).
 
    Baada ya kuruhusiwa na Farao kutoka Misri Musa akaanza kuwaongoza Waisraeli kuelekea Nchi ya Kaanani ambayo aliwaahidi Waisraeli. Waisraeli waliishi Misri miaka 430.
 
    Waisraeli walisafiri miaka 40 Jangwani wakielekea Nchi ya Kaanani. Mungu aliwaongoza Waisraeli kupitia Musa. Awali Waisraeli waliambiwa watakapofika katika Nchi ya Kaanani na Miji yake waue watu wote wasimuache hata mmoja, bali wabakize wanyama tu.
 
    Musa hakuendelea kuliongoza Taifa la Israeli kwa kuwa alikuwa mzee na hivyo
hakufika katika Nchi ya ahadi. Alikufa akiwa miaka 120 na kuzikwa katika Nchi ya
Moabu na Yoshua mwana wa Nuni akashika usukani wa kuliongoza taifa la Israeli
kuelekea Nchi ya hadi.
 
    Walipofika katika Nchi hiyo kwanza wakatuma wapelelezi waende kupeleleza Nchi
hiyo ambapo walifikia kwa mwanamke mmoja aliyeitwa Rahabu.Upelelezi ulipokamilika
kazi ya kuupiga mji huo ikaanza.
 
   Waisraeli wakiongozwa na Yoshua wakiipiga miji ya Nchi hiyo kwa makali ya upanga.
Waliteka miji ya Hai, Yeriko na Yordani. Awali kabla ya mapambano Yoshua
aliwaambia Waisraeli kama watayasikiliza maneno ya Mungu basi Mungu atawatia
Wakaanani mikononi mwao (Yoshua 3:9-10).
 
    Yoshua akaipiga Nchi yote na kuiteka sawasawa na neno la Mungu, baada ya kuitwaa akawagawia Waisraeli urithi wao kama walivyoambiwa na Mungu (Yoshua 12:6-23).
 
    Lakini kitu kikubwa walichokosea Waisraeli ni kuwabakiza Wakaanani, yaani Wapalestina wa leo ambao wanasuguana nao leo.
 
    Katika vita hiyo mji mgumu kuuteka ulikuwa Yerusalemu ambao leo ndio unaopiganiwa sana na Wapalestina na Waisraeli kila mmoja akidai ni wa kwake. Ukiondoa Misaafu ya dini, hata vitabu vya kihistoria vinalizungumzia suala la vita hii jinsi ilivyokuwa ngumu katika kuishinda Mji wa Yerusalemu kwani  kwa uwezo wa Mungu Yoshua aliamuru Jua lisimame na likasimama bila kuzama hadi Waisraeli waliposhinda.
 
    Mfalme wa Yerusalemu aliyeitwa Adoni-Sedeki aliposikia Yoshua ameishinda Miji mingine akaungana na Wafalme watano wa Wapalestina kupambana na waisraeli ili wasije wakauteka Mji wa Yerusalemu. Kufuatia kuungana huku vita ikawa kali sana kati ya Waisraeli na Wakaanani (Wapalestina).
 
    Wakati vita ikiendelea kupiganwa jua lilikuwa likikaribia kuzama na desturi ya enzi zile ni kwamba vita inapopiganwa linapozama jua, basi vita hutulia kwa kitambo hadi kesho yake hivyo Yoshua akachukua jukumu la kumuomba Mungu asimamishe jua hadi wao washinde. Jua lilizama baada ya Waisraeli kuushinda mji wa Yerusalemu. (Yoshua 11:1-23).
 
    Katika miji mingine Waisraeli waliwauwa Wapalesttina wote isipokuwa katika miji ya Gath , Ashdodi na Gaza ambako kuna makazi ya Wapalestina hata hivi leo. (Yoshua 11;22). Licha ya kuwaacha Wapalestina lakini Waisraeli walifanya mapatano na Wapalestina suala ambalo lilikatazwa na Mungu.
 
    Mungu aliwaambia Waisraeli kwa sababu wamefanya mapatano na Wapalestina basi Wapalestina watakuwa miiba mbavuni mwao na hatawafukuza watoke mbele zao (Waamuzi 2:1-3).
 
    Lakini hata hivyo Misaafu ya dini inajichanganya yenyewe kwa mfano katika Biblia Kitabu cha Waamuzi 3:1, kinasema “Basi hayo ndiyo Mataifa ambao Bwana aliwaacha ili awajaribu Israeli kwa hao yaani awajaribu hao wote ambao hawakuvijua vita vyote vya Kaanani, ili kwamba vizazi vya Israeli wapate kujua, ili kuwafundisha vita, hasa wao ambao hawakuvijua vita kabla ya wakati ule, aliwaacha wakuu watano wa Wafilisti (Wapalestina) Wakaanani wote na Wasidoni na Wahivi waliokaa katika kilima cha Lebanoni toka mlima wa Baal-Hermoni mpaka kuingia Hamathi.
 
    Awali kabisa Waisraeli waliishi Kaanani (Palestina) na kisha walienda Misri baada ya Kaanani kukumbwa na njaa. Baada ya kuibuka Farao mpya Nchini Misri, asiyemtambua Yusufu Waisraeli walianza kuteswa na kisha kurejea katika Nchi waliyodai ya kwao yaani Nchi ya Kaanani ambayo ndiyo Izraeli ya leo.
 
    Mgogoro wa Wapalestina na Waisraeli unakuwa mgumu kwa sababu Waisraeli wanaamini Palestina ni Nchi yao waliyoahidiwa na Mungu na Wapalestina kwa upande wao wanaona wamevamiwa katika Nchi yao kama Biblia inavyosema kwamba Wapalestina watakuwa miiba kwa Waisraeli na ndivyo ilivyo hivi sasa.
 
Kitabu cha GLOBAL  INSIGHTS, People and Cultures kilichoandikwa na Waandishi wanane baadhi yao wakiwa Maprofesa waliobobea katika masuala ya historia, kinasema kuwa Wayahudi wanaami kuwa wao ni Taifa teule na kwamba Masiha atatoka katika Taifa lao na kwamba katika Taifa hilo wakati Yesu akizaliwa lilikuwa likitawaliwa na Warumi(ukurasa wa 33 na 34).
 
Katika ukurasa wake wa 48 kitabu hicho kinaeleza kuwa Waaraabu waligawanyika katika Makundi ya Wakaanani,Wafilisti na Wamisri na wote wakaja kuwa Waarabu kwa kijifunza kiarabu.Kumbuka msomaji kwamba Wakanani  ndio Wapalestina wa leo.Pia kitabu hicho kinaelea kuwa asilimia 90 ya Waarabu ni Waislamu.
 
    Wapalestina wanaishi kama wakimbizi katika Nchi ya Israeli kwa mujibu wa kitabu cha Global Insights, people and cultures ni kwamba zaidi ya Wapalestina Milioni mbili wanaishi nje ya Israeli katika makambi yao huko Yordani na wengine wanaishi katika ukanda wa Gaza chini ya Waisraeli na wengine  milioni moja wanaishi Israeli.
 
    Kwa mujibu wa kitabu hicho ni kwambaWapalestina watajisikia furaha na matumaini ikiwa watarejeshewa Nchi yao toka kwa Waisraeli na kutambuliwa kama Taifa huru la Kipalestina. Wapalestina wamekata tamaa kufuatia kunyanyaswa na Waisraeli na sasa wanaamua kuwafundisha watoto wao kushika bunduki na kujilipua wenyewe ili mradi wameua Waisraeli kadhaa.
 
 Kitabu hicho cha Global Insight, people and Cultures kinawaonyesha watoto wa kipalestina wenye umri kati ya miaka 5 hadi 7, wakiwa wamevalia nguo za kijeshi, wakifundishwa kupambana na maadui zao Waisraeli.
 
    Kwa mujibu wa kitabu hicho ni kwamba licha ya matatizo wanayokumbana nayo Wapalestina. Wanaamini wao ni Wapalestina. Wanafunzi wa kipalestina wanafundishwa kuamini suala hilo . Wanafunzi wanafundishwa kuamini kwamba wao sio Wamisri au Waarabu wa sehemu nyingine bali wao ni Wapalestina.
 
    Kwa mujibu wa kitabu hicho ni kwamba mgogoro baina ya Wapalestina na Waisraeli ulianza mara baada ya kuundwa Taifa la Israeli, Mei 14, 1948. Kitabu hicho kinasema Waarabu hawakupendezewa na kuundwa kwa Taifa hilo hivyo wakaamua kukungana ili kuliangamiza Taifa hilo ambapo Waarabu walishindwa vibaya katika mapambano hayo.
 
    Kitabu hicho kinasema zaidi ya wapalestina Milioni 2 wanaishi nje ya Israeli, wengi wao wanaishi kwenye makambi ambayo yako katika hali ya kimaskini. Kitabu hicho kinasema makambi hayo yana vibanda ambavyo Wapalestina wanaishi watu tisa tisa katika vibanda hivyo. Wapalestina wengine Milioni 1 wanaishi katika ukanda wa Gaza chini ya utawala wa Waisraeli na nusu milioni wanaishi Israeli.
 
    Kitabu hicho kinabainisha kwamba kuna waisraeli Milioni tatu na nusu katika Nchi ya Israeli ambao wengine walitokea Uingereza, Mashariki ya Kati, Afrika Kaskazini, Asia na Amerika Kusini na Kaskazini na wanaunganishwa na dini ya Uyuda.Wanaamini kwamba Israeli ni Nchi yao ambayo Mungu aliahidi kuwapa. Lugha wanayotumia ni kiebrania(Global Insights, People and Cultures page 50-53)
 
    Waisraeli na Wapalestina wanashindwa kuelewana kwa sababu ni watani wa jadi ambapo wamekuwa wakipambana mara kwa mara katika Historia yao yote ambapo kama ukisoma Biblia katika kitabu cha samweli 17:1-58, utaona mapambano baina ya Daudi Muisraeli na Goliathi shujaa wa vita wa wapalestina. Inakuwa vigumu Wapalestina kujikwamua kwenye makucha ya waisraeli kwa sababu Mungu alisema Nchi hiyo amewapa Waisraeli   kama alivyowaahidi na Waisraeli kwa upande wao wanavuna walichokipanda kwani Mungu aliwaagiza kuwaangamiza wapalestina wao wakawaacha.
 
    Baadhi ya Wachambuzi wa masuala ya kidini wanasema kuwa Biblia inasema Nchi ya Israeli ni Nchi halali ya Waisraeli kwa kuwa waliishi mwanzo na kisha kwenda Misri baada ya njaa kuingia katika hiyo na wakarejea tena kama Mungu alivyowaahidi na kwamba mgogoro huo hautakwisha hadi Yesu atapokuja mara ya pili.
 
    Hivyo basi katika kutatua mgogoro wa Wapalestina na Wayahudi hekima na busara zaidi inatakiwa ikibidi kurejea kwenye vitabu vya dini vya Korani na Biblia na kisha kuchanganya na Siasa. Hata hivyo viongozi wa kimataifa wanaposuluhisha mgogoro huo wajaribu kutafakari kifungu kwamba Mungu aliwabakiza Wapalestina ili kuwafundisha Vita Waisraeli vinginevyo watakuwa wanaponda maji kwenye ikunu kaika kutatua nmgogoro huo wa Mashariki ya kati
 
Kwa mtizamo wangu katika mgogoro huu unaoendelea busara zaidi zinapaswa zitumike katika wakati huu ambapo baadhi ya Wasomi wamekuwa wakiibuka na kuitaka Israeli iache kuikalia Palestina na kwamba iwaachie Wapalestina Nchi yao .
 
    Wasipotumia akili wanaweza wakawa wanatumia pesa nyingi kutatua mgogoro ambao hauishi na ambao ulitabiriwa kwamba Wapalestina waliwekwa kwa ajili ya kuwafundisha vita Wayahudi na kwamba vita hivyo vitamalizwa na Mungu mwenyewe.
 
MWISHO.
 Mwandishi wa makala hii ni mchambuzi wa masuala ya kisiasa,kijamii na kimataifa
Anapatikana kwa simu namba – 0755/0655 761195Barua pepe – josephmwambije@yahoo.co.uk

1 comment:

  1. AHSANTE mwandishi kwa maelezo mazuri.

    Haipingiki nchi ya Kanaani ni mali ya Israel kwa sababu kihistoria;
    1.Waliahidiwa na kupewa waikalie milele

    2.Kwa sababu zisizoepukika
    (mf. njaa,kutekwa n.k) Waisrael waliondoka kwao kwenda ugenini
    =>Muda huu ndipo waarabu wakajiimarisha hapo

    SASA WENYE NCHI WAMERUDI
    Nao ni waIsrael
    3.

    ReplyDelete