Wednesday, July 25, 2012

KUNA UKWELI GANI KUHUSU MWISHO WA DUNIA?


NA JOSEPH MWAMBIJE

   KATIKA miaka ya hivi karibuni watu wamekuwa wakiishi kwa hofu kutokana na tabia za watu mbalimbali ambao wamekuwa wakitabiri kuhusiana na mwisho wa dunia na kwamba Sayansi ya Dunia iko ukingoni.

   Tabiri hizi zimekuwa zikiweka watu njia panda ambapo wengine wamekuwa wakitafakari ikiwa Yesu au Issa bin Mariam atakuja watajibu nini ilhali hawana maandalizi yoyote lakini wengine wenye mioyo dhaifu wanadiriki kuacha shughuli zao na kumsubiri Yesu huku wengine wakienda milimani kusubiri ujio wake.

   Mwaka jana tulishuhudia vituko zaidi vya vikundi vya watu waliowaachisha watoto wao shule na kwenda milimani kusubiri ujio wa Bwana Yesu na wengine wakitaka kwenda Ulaya kuhubiri injili bila kuwa na paspoti na tiketi za Ndege kwa madai kuwa mwisho wa dunia umefika.

   Lakini taarifa za hivi karibuni ambazo zimedai kuwa ifikapo Disemba 21 mwaka 2012 ni mwisho wa dunia zimezua hofu zaidi kwa wakazi wa dunia, hofu inatanda zaidi kutokana na kauli za Wanasayansi wanaodai kuwa Sayari ya dunia hii imebakiza miezi michache kufikia ukomo wake.

   Kauli za Wanasayansi hao zinasimamia kwenye vipimo vya tabiri za mnajimu wa Kifaransa, Michael de Nastredame aliyeishi karne ya 16 (1503 – 1566),  tabiri za mnajimu huyo maarufu kupitia kitabu chake cha Les Prophetics (Ubashiri) zinadai kuwa mwaka 2012 kutakuwa na vita ya tatu ya dunia itakayosababisha maangamizi makubwa ya dunia.

   Kutokana na utabiri huo Wanasayansi walio katika mlengo wa kat ya Sayansi na Unajimu wanayajengea hoja maandishi ya Nostradumus kuwa uwepo wa Nishati za Nyuklia katika Nchi mbalimbali ndiyo zao la dunia wakati wa Vita Kuu ya tatu. Kwa wale wanaofuatilia makala zangu kuna wakati niliwahi kuandika Makala yenye kichwa, Mzozo wa Israel na Irani na hofu ya kuzuka Vita ya tatu ya dunia.

   Baadhi ya Nchi zinazomiliki Nishati ya Nyuklia ni Marekani, baadhi ya Nchi zilizokuwa zinaunda Umoja wa Soviet , China , Ufaransa , India , Pakistan , Iran na Korea Kaskazini.    Athari za mabomu ya Nyuklia zipo Hiroshima Nchini Japan ambapo athari zake zipo hadi leo kutokana na bomu hilo la Atomic lililotupwa wakati wa Vita ya Pili ya dunia mwaka 1939 hadi mwaka 1945.

   Kutokana na makali ya Bomu hilo ambalo liliua watu 80,000 na wengine wengi kujeruhiwa Japan ilisalimu amri na vita hiyo ikakomeshwa, katika Mji wa Hiroshima ambako lilitupwa bomu hilo hadi leo bado watu wanazaliwa vilema huku kukiwa na simanzi isiyofutika. Nchi za Israel , Afrika Kusini , Argentina na Brazil zinatajwa kuwa na uwezo wa kumiliki na kutumia Nyuklia lakini bado hazina mpango wa kumiliki na kurutubisha silaha hizo za maangamizi.

   Wanasayansi wanaeleza kuwa kizaazaa cha dunia kuangamia ni tufani zito ambalo litaigonga na kusababisha kupoteza mawasiliano kati yake na jua hivyo ile sumaku ya asili kushindwa kufanya kazi yake, katika maelezo yao wanasayansi wanafafanua kuwa kuna Sayansi inayoitwa Nibiru Planet x ambayo itapoteza mwelekeo Disemba 21 2012na kuigonga dunia na kusababisha itoweke.

   “Hii ina maana kuwa baada ya Disemba 21, 2012 hakutakuwa na Sayansi inayoitwa dunia kwani itagongwa na Planet x na kuipoteza, itaiachanisha na jua kisha itadondoka”  ilisema sehemu ya ripoti ya Wanasayansi hao.

   Hata hivyo kwa upande wa pili Wanasayansi  wa Taasisi ya NASA ya Nchini Marekani wanautaka Ulimwengu kutambua kwamba 2012 si mwisho wa dunia huku wakiwataka wakazi  wa dunia kutokuwa na wasiwasi kuhusiana na habari za mwisho wa dunia. NASA wanadai kuwa katika matoleo yote yanayoelezea kuwa dunia mwisho wake ni 2012, hakuna hata moja ambalo wamejiridhisha kitaalamu badala yake wameelezea hali hiyo kwamba inakuja kwa lengo la kutisha watu.

   Habari za mwisho wa dunia hazijaanza leo ambapo iliwahi kuelezwa kuwa mwaka 1844 ni mwisho wa dunia, pia ikaelezwa kuwa mwaka 2000 ni mwisho wa dunia lakini pia ikavumishwa kuwa mwaka 2003 ndio ingekuwa ukomo wa dunia. Pia kumekuwa na watu wengi ambao wamekuwa wakiibuka na kujitangaza kuwa wao ni Yesu.

   Lakini hebu twende kwenye hoja za msingi katika biblia na vitabu vingine vya dini tuone ukweli uko wapi, madai hayo ya mwisho wa dunia yana ukweli gani? Je Biblia inawaitaje wanazusha kuhusu mwisho wa dunia na kwamba matukio yanayotendeka sasa yanaashiria nini?

   Hofu imetanda huku baadhi ya maeneo wakishindwa hata kufanya kazi wakijiandaa na mwisho wa dunia, kwingineko duniani wameuza walivyonavyo na kusaidia maskini kisha kubaki watupu wakisubiri ujio wa Yesu kwa hofu kuu wakiwa na hoja kwamba mali wanazomiliki hazina maana wakati dunia imefika mwisho, lakini pia ndani ya biblia tutaona kama hayo ni maagizo ya Yesu.

   Watu waishi kwa hofu wakihofia mwisho wa dunia, pia tutaona kama kuna tarehe, mwezi na mwaka vilivyotajwa kuwa ni mwisho wa dunia na Ujio wa Yesu? Naam kwa wale wasiyoyafahamu Maandiko Matakatifu.wanakuwa na hofu kubwa hadi kufikia kiwango cha kupatwa shinikizo la damu au ugonjwa wa moyo wakihofia mwisho wa dunia.

   Katika hofu zao ndipo na matapeli wanawajia wakidai  wakidai wao ni akina Yesu na Manabii waliotumwa na Mungu  kuja kuwapa maonyo na kuwataka kukabidhi mali zao kwa akina Yesu hao na Manabii hao wa Uongo. Katika miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia akina Yesu wengi wa uongo na Manabii wa uongo.

   Dunia bado haijasahau yale yaliyotendwa na Nabii wa uongo Bw. Kibwetere na kule Uganda aliyewaamuru wafuasi wake wamkabidhi mali zake na kusubiri mwisho wa dunia wakiwa kanisani, mwisho uliowajia kwa Nabii huyo wa uongo kuwachoma moto wakiwa kanisani na familia zao.

   Mikanganyiko hii itazidi kuwaathiri wengi wasioyafahamu maandiko kadri tunavyosonga mbele huku akina Yesu wa bandia wakizidi kuibuka na kutoa mafundisho kinyume na Yesu wa ukweli ambaye kwa mujibu wa Biblia yuko mbinguni akiwaombea watu wake pengine hili suala la mwisho wa dunia au kiama ni suala tete ambalo halina budi kujadiliwa kwa kuwa linatugusa katika maisha yetu ya kila siku.

   Nasema linatugusa kwa kuwa kila binadamu kuna kitu anachoabudu na katika hilo wapo wapagani ambao hawana dini, wapo wanaoabudu dini za jadi na wapo wanaoabudu dini mbalimbali lakini katika yote Biblia inasema kitu chochote ambacho mwanadamu anakiweka mbele kuliko Mungu basi huyo ndiye Mungu wake hivyo basi kwa mantiki hiyo hakuna ambaye hana Mungu.

   Ili kupata ukweli wa tarehe, mwezi, mwaka na siku sahihi ya kuja Bwana Yesu na mwisho wa dunia hebu tuiulize Biblia inayoaminiwa na wakristo wengi na wasio wakristo duniani. Biblia inasema katika kitabu cha Mathayo 24:3 – 6, Hata alipokuwa meketi katika mlima wa Mizeituni Wanafunzi wake wakamwendea kwa faragha wakisema tuambie mambo hayo yatakuwa lini, nayo ni nini dalili ya kuja kwako na ya mwisho wa dunia? Yesu akajibu akawaambia, angalieni mtu asiwadanganye kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu wakisema mimi ni Kristo, nao watawadanganya wengi, nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya Vita, angalieni msitishwe, maana hayo hayana budi kutokea, lakini ule mwisho bado.
   Hapa tunaona kwamba habari za mwisho wa dunia hazijaanzia kwetu, kumbe zilianza toka kwa wanafunzi wa Yesu ambao walitaka kujua ukweli wa Mambo hayo, wanahoji mambo hayo yatakuwa lini na dalili za kuja kwa Yesu na mwisho wa dunia?  Lakini Yesu anajibu kwamba waangalie mtu asiwadanganye kwa sababu wengi watakuja wakidai wao ni akina Kristo na kwamba watawadanganya wengi na pia anawaambia watayasikia matetesi ya Vita wasitishwe kwani ule mwisho bado.

   Pia Yesu anatahadharisha kuwa tusitishwe kwa kuwa tutasikia Matetesi ya vita lakini mwisho wa dunia bado. Hapa Yesu anagusia dalili za kuja kwake na mwisho wa dunia kuwa ni pamoja na matetesi ya Vita na kuthibitisha kuwa kuna mwisho wa dunia lakini hauji kiuzushi kama watu wanavyozusha hivyo bado anawaasa watu kutokuwa na hofu na ujio wake.

   Ukiendelea katika mstari wa 7 katika kutaja dalili za ujio wake na mwisho wa dunia anasema Taifa litaondoka kupigana na Taifa, Ufalme kupigana na Ufalme, kutakuwa na njaa na kutakuwa na matetemeko ya Nchi na mahali mahali. Dalili hizi zinazoelezwa na Biblia zimetokea sana na kukaririwa katika bongo za watu wengi ambapo hadi hivi leo dunia imeshuhudia vita nyingi sana na ni nchi chache sana duniani ambazo hazijawahi kupigana Vita.

   Matetemeko ya ardhi ndio usiseme na hivi karibuni lilitokea tetemeko la ardhi Nchini Haiti na kuua watu wengi, upande wa njaa Nchi nyingi duniani zinakumbwa na njaa na watu wanakufa kwa njaa. Katika mstari wa 11 Yesu anasema Manabii wengi wa uongo watatokea ns kuwadanganya wengi. Kuhusu Manabii wa uongo nimekwisha kueleza na nikagusia kuhusu akina Kibwetere.

   Pia katika sura hiyo ya Mathayo 24 anasema kwa sababu ya kuongezeka Maasi upendo wa wengi utapoa ambapo katika hili tumeshuhudia ndugu wakiuana kwa sababu ya mali huku wengine wakiwatoa watoto wao kafara kwa kuuwaua kikatili kwa sababu ya mali .

   Ukifuatilia vyombo vya habari ndugu msomaji kuna mambo mengi ya kutisha yanayofanywa na wanadamu ambayo hata Shetani mwenyewe yanamshangaza. Nimewahi kusoma simulizi ya jamaa mmoja aliyeuwa watoto wake wawili, mama yake na kisha kuzini na maiti ya Msichana mrembo aliyemuua ili apate utajiri. Ni simulizi ya kutisha ambayo Jamaa huyo alizini na maiti inayotoa harufu huku sauti ya Jini ikimwambia atakuwa milionea kwa kutimiza masharti ya kishirikina.

   Anasema wakati huo mtu akiwaambia tazama, kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki kwa maana watatokea Makristo wa wa uongo na Manabii wa uongo nao watatoa ishara kubwa na maajabu wapate kuwapoteza yumkini hata walio wateule. Labda nihoji, hadi naandika Makala hii kuna Yesu wangapi wa uongo waliokwishaibuka? Bila shaka ni wengi.

   Biblia inaendelea kusema “Tazama nimekwisha kuwaonya mbele, basi wakiwaambia, yuko jangwani msitoke, yumo nyumbani msisadiki, kwa maana kama vile umeme utokavyo  Mashariki ukaonekana hata Mangharibi hivyo ndivyo kutakavyokuja kwake Mwana  wa Adamu.

   Hiyo ni hoja ya msingi sana kwamba Yesu atapokuja ataonekana na watu wote kama vile Umeme kwani huko mbele tutashuhudia maajabu makubwa zaidi ya haya tunayoyaona ambapo shetani ataigiza kuja kwa Yesu na kutoa maagizo yaliyo kinyume na Mungu huku akihalalisha na kubariki uovu.

   Yesu atapokuja ataonekana na watu wote lakini Yesu huyu wa bandia ataonekana baadhi ya maeneo. Mathayo 24:36  inasema “Walakini kwa habari ya siku ile na saa ile hakuna ajuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana (Yesu)  ila baba(Mungu) peke yake. Sasa nihoji hao wanaotabiri kwa kutaja tarehe, mwezi, siku na mwaka wa kuja yesu uhakika huo wanautoa wapi wakati Biblia inasema hata Yesu mwenyewe hajui.

   Lakini hoja ya msingi Biblia inasema wanadamu wanapaswa kujiandaa na ujio wa Yesu kwa kuwa hawajui atakuja lini ambapo Mathayo 24: 42 anasema “kesheni basi kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana (Yesu) wenu. Ifahamike kuwa kukesha kunakoelezwa hapa si kukesha kwa kukaa macho la hasha bali kuwa tayari kwa kutenda mema muda wote. (Biblia katika sura ya 24 ya Mathayo)

   Kauli hii ya Yesu inashabiina na usemi maarufu sana usemao ishi katika maisha ya dunia kana kwamba utaishi miaka 100 ijayo na kidini ishi kama utakufa leo, kauli hiyo inamaanisha kwa maisha ya kidunia fanya mambo ya maendeleo kwa matarajio ya kuendelea kuwepo duniani muda mrefu na kwa maisha ya dunia ujiandae kana kwamba utakufa leo.

   Kikubwa tunachopaswa kutambua ni kwamba dalili nyingi za kuja kwa Yesu na mwisho wa dunia zimetimia na zinaendelea kutimia na kwamba yuko jirani kuja na si kwamba ule mwisho umefika bali “U karibu kufika, lakini pia hawapaswi kuishi kwa hofu kwani Yesu ni mtu wa upendo.
   Ifahamike kuwa dunia haitaangamizwa kwa Vita kama wanasayansi wanavyodai na pia mwisho wa dunia hautakuja kwa dunia kugongana na Sayari nyingine bali itaangamizwa kwa moto kwa maana watenda mabaya wataangamizwa kwa moto ( Ufunuo 20: 12 – 15) Ikumbukwe pia dunia ya kwanza wakati wa Nuhu iliangamizwa kwa maji na baada ya dunia kuangamizwa kutakuwa na Mbingu mpya na Nchi mpya na Mji mtakatifu Yerusalemu piya utaoshuka kutoka Mbinguni (Ufunuo 21: 1 – 2)

MWISHO.
Mwandishi wa Makala hii anapatikana kwa simu-0755/0655 761195
Barua pepe-josephmwambije@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment