Friday, June 7, 2013

RASIMU YA KATIBU MPYA :MAWAZIRI KUKAIMU URAIS

.Ni mapendekezo ya Rasimu ya katiba mpya


  Makamu wa Rais Dkt Gharib Bilali akionyesha Rasimu ya Katiba mpya kabla ya kuizindua Jijini Daressalaam.Wa kwanza  kulia ni Waziri Mkuu wa Tanzania,Mizengo Pinda.Wa kwanza  kushoto ni Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mpya  Joseph Warioba na anyemfuatia ni Makamu wa kwanz wa Rais Zanzibar Seif Sharif .

HABARI KAMILI......

 Kutokana na rasimu ya Katiba Mpya kupendekeza kufutwa kwa nafasi ya Waziri Mkuu, rasimu hiyo inapendekeza waziri yeyote mwandamizi ateuliwe kukaimu nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa rais na makamu wake hawapo nchini kutokana na sababu zozote zile.
Mapendekezo hayo ni tofauti na Katiba ya sasa ambayo inatamka kwamba ikiwa Rais na Makamu wake hawapo, basi nafasi hiyo ya juu katika nchi itashikwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Waziri Mkuu aliwekwa katika orodha ya wanaoweza kukaimu nafasi hiyo katika marekebisho ya Katiba yaliyofanywa mwaka 2000 kupitia waraka maalumu wa Serikali (white paper) na baadaye kupitishwa na Bunge.
Kabla ya marekebisho hayo ya 13, Ibara ya 37(3)(a) na (b) ilikuwa ikieleza kuwa iwapo Rais na Makamu wake hawapo nafasi hiyo ilitakiwa kushikiliwa na Spika wa Bunge na kama hayupo basi Jaji Mkuu wa Tanzania ndiye alitakiwa kukaimu nafasi hiyo.
Lakini mapendekezo ya Rasimu ya Katiba Mpya katika Ibara ya 73(1)(b)na (c) inaeleza kuwa endapo Rais na Makamu wake hawatakuwapo basi nafasi hiyo itashikiliwa na waziri mwandamizi na kama hatakuwapo basi Baraza la Mawaziri ndilo litakalokuwa na dhamana ya kuchagua mtu wa kukaimu nafasi hiyo.
Hata hivyo, mtu yeyote atakayekaimu nafasi ya madaraka ya Rais, kwa namna yoyote ile, hatakuwa na madaraka ya kuteua au kumwondoa madarakani kiongozi yeyote yule aliyeteuliwa na Rais kwa mujibu wa Katiba au jambo jingine lolote kama litakavyoainishwa na Rais katika hati ya kukasimu madaraka yake.
“Rais atakasimu madaraka yake kwa hati maalumu aliyotia saini yake,” inaelekeza rasimu hiyo iliyozinduliwa Jumatatu wiki hii na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.
Kadhalika rasimu hiyo inaeleza kuwa endapo Baraza la Mawaziri litaona kuwa Rais hawezi kumudu kazi zake kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili, linaweza kuandaa azimio la kumwomba Jaji Mkuu athibitishe kwamba Rais, kwa sababu ya maradhi ya mwili au ya akili, hawezi kumudu kazi zake.
“Baada ya kupokea azimio hilo, atateua bodi ya utabibu ambayo itachunguza suala hilo na kumshauri Jaji Mkuu ipasavyo,” inaelekeza rasimu hiyo.
Jaji Mkuu baada ya kutafakari ushauri na ushahidi wa kitabibu, atampelekea Spika hati ya kuthibitisha kwamba kutokana na maradhi ya mwili au akili, Rais ameshindwa kumudu kazi zake, na iwapo Jaji Mkuu hatabatilisha hati hiyo ndani ya siku saba kutokana na Rais kupata nafuu na kurejea kazini, basi itahesabiwa kwamba kiti cha Rais kipo wazi.
Kutokana na hali hiyo, bodi ya utabibu itakayoteuliwa kwa mujibu wa Katiba itajumuisha watu wasiopungua watatu kutoka miongoni mwa madaktari bingwa wanaotambuliwa na sheria inayohusu madaktari ya Tanzania.
“Endapo kiti cha Rais kitakuwa wazi kutokana na Rais kufariki dunia, kujiuzulu, kupoteza sifa za uchaguzi, kutomudu kazi zake kutokana na maradhi ya mwili au akili au kushindwa kutekeleza kazi na shughuli za Rais, basi Makamu wa Rais ataapishwa na kushika madaraka ya Rais kwa muda uliobaki katika kipindi cha miaka mitano,” inaeleza sehemu nyingine ya rasimu hiyo.

CHANZO-MWANANCHI

No comments:

Post a Comment