Wednesday, December 19, 2012

MAZOEZI KABALA YA KUPATA KIFUNGUA KINYWA HUBORESHA AFYA


Mazoezi na Furaha
Daktari mmoja aitwaye Mackod, alipitia makala nyingi za afya ili kuweza  kutambua visababishi vya vifo ambayo havitokani na umri au nasaba ya kiasili (genetic), na akagundua mambo tisa ambayo yanasabisha vifo ambavyo vingeweza kuzuilika.

Mambo hayo tisa ni; uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe, ukosefu wa mazoezi, lishe duni, wadudu kama bakteria na virusi, ajali, tabia za ngono za kupita kiasi bila kinga,  vita na madawa ya kulevya.
Katika makala hii ningependa kuzungumzia juu ya ufanyaji wa wazoezi na hasa wakati bora wa kufanya mazoezi.

Mazoezi ni muhimu sana kwa ajili ya kupunguza mafuta ya ziada mwilini, tafiti zinaonesha kuwa asiyefanya mazoezi, madhara anayopata ni sawa na mtu anayevuta tumbaku.
Utafiti uliofanywa na Dr. Jason na Nor Farah (2004) wa Chuo kikuu cha Glasgow, umeonesha kuwa unapofanya mazoezi kabla ya kifungua kinywa, wakati tumbo likiwa tupu, ni bora zaidi kuliko unapoweza kufanya mazoezi baada ya mlo wowote. Kufanya mazoezi ni jambo la maana kwa afya kuliko kutokufanya mazoezi ya mwili, lakini unaweza kupata  faida zaidi kama unaweza kufanya kabla hujala chochote.
Mazoezi kwa ujumla wake yana umuhimu mkubwa kwa afya ya binadamu, hasa kama yakiambatana na lishe bora.

Mazoezi huweza kuzuia magonjwa sugu kama kisukari, magonjwa ya moyo, kansa na shinikizo la damu, pia kwa kufanya mazoezi unaweza kuongeza kipato kwa kuwa unaweza kufanya kazi muda mrefu kuliko asiye fanya mazoezi.

Familia ambazo hufanya mazoezi huwa na afya bora na kipato kikubwa kwa kuwa fedha kidogo wanazopata hutumika kwenye maendeleo ambapo familia wasiofanya mazoezi, hujikuta wakitumia kipato hicho kidogo kwa ajili ya magonjwa ambayo yangeepukika kwa kufanya mazoezi.
Pia kwa kufanya mazoezi kila mara na hasa kabla ya mlo kuna faida nyingi ambazo haziwezi kuonekana kwa haraka, kama vile kuimarisha hali ya kiakili, ambayo matokeo yake ni kuwa na furaha.

Hii inatokana na kuzalishwa kwa wingi kwa kemikali aina ya endorphins wakati wa kufanya mazoezi.

Kemikali hii ya  endorphins  ni muhimu kwenye mapambano ya sonono (depression) na hivyo kumfanya mfanya mazoezi kuwa na furaha zaidi.

Tafiti zinaonesha kuwa mwili huzalisha kemikali hii ya endorphins baada ya mtu kufanya mazoezi ya kawaida kwa dakika 12.

Kama wanafamilia wanaweza kufanya mazoezi kwa muda hata wa saa moja, au nusu saa, wanaweza kuwa na furaha na kuzuia kusambaratika kwa ndoa zao.
Mazoezi na Furaha
Pia kuna kemikali nyingine muhimu ambayo tafiti zinaonesha kuwa huzalishwa baada ya kufanya mazoezi.

Kemikali hii itwayo “serotonin” huongezeka kwenye mfumo wa neva baada ya kufanya mazoezi, ambayo hufanya mfanya mazoezi ajisikie vizuri kiafya na kupunguza sonono (depression). Tafiti pia zinaonesha kuwa kemikali hii, ni muhimu sana katika mwili, kwani hufanya mfanya mazoezi alale usingizi mnono.
Ufanyaji wa mazoezi mara kwa mara husaidia pia mfanya mazoezi ajithamini, na kuondoa uchovu na unyonge. Unapojithamini, pia inaleta tokeo ya kujiona bora na kuwa mwenye ustawi. Mazoezi pia hufanya tendo la ndoa kuwa bora na hivyo kuleta mahusiano bora ya kinyumba na mpwendwa wako.
Nimejaribu kuanisha umuhimu na faida za maozezi  na hasa wakati  yanapokuwa na tija ili kuleta hamasa ya kufanya mazoezi kwa kila msomaji wa makala hii. Unaweza kufanya mazoezi wewe na familia yako au na wenzako, au pekee yako, chukua muda kidogo katika masaa 24 na ufanye mazoezi, maana utajisikia vizuri na kuwa mwenye afya, lakini kumbuka utapata faida zaidi ukifanya mazoezi wakati tumbo likiwa tupu, yaani kabla ya mlo, baada ya kula chakula tembea taratibu ili kukifanya kitulie vema tumboni.
Usisahau, kabla ya kifungua kinywa asubuhi jitahidi ufanye mazoezi angalau kwa muda wa robo saa.
CHANZO-MTANDAO WA DULLONET

No comments:

Post a Comment