Tuesday, January 1, 2013

WATANZANIA WAFIKIA MILIONI 45 KUTOKA MILIONI 34.4


 HABARI KAMILI
Daressalaam
Rais Jakaya Kikwete akitangaza matokeo ya sensa ya mwaka 2012 jana jijini Dar es salaam

Rais Kikwete alisema Sensa hutoa taarifa muhimu zinazotumiwa na Serikali kupanga mipango ya maendeleo ya watu wake.
“Tulitenga siku 14 kwa ajili ya zoezi hili la Sensa, wengine hizi ndizo walifanya siku za mikutano na maandamano. Mwaka una siku nyingi, lakini sijui kwa nini walitaka wafanye mikutano na maandamano hayo katika siku hizi 14 tu?” alisema Rais Kikwete.
Aliwashukuru viongozi wa vyama vya siasa, dini na vyama vya kiraia pamoja na wamiliki wa vyombo vya habari ambao waliwahamasisha watu wao kushiriki katika sensa hiyo akiwataka kuendelea kuhamasisha matumizi ya taarifa za matokeo ya Sensa hiyo.
Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Sensa hiyo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alisema Serikali kutokana na kutambua umuhimu wa Sensa, imekuwa ikiongeza bajeti kwa ajili ya shughuli hizo.
Alisema katika Sensa ya mwaka huu, imetoa asilimia 90 ya gharama zote, kulinganisha na asilimia 75 katika Sensa ya mwaka 2002.
Alisema pia katika kutekeleza jukumu hilo kulikuwa na changamoto mbalimbali ikiwamo ya watendaji wanne kupoteza maisha. Hata hivyo, hakufafanua zaidi walipoteza maisha katika mazingira yapi.
Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema Sensa ya mwaka 2012, itachangia kuboresha maisha kwa kutumia takwimu sahihi za wakati ili kuwezesha kutunga sera na kupanga maendeleo.
Alisema matokeo ya Sensa ya 2012 yametoka mapema kuliko miaka mingine kutokana na maendeleo ya kiteknolojia na utayari wa Serikali katika kuhakikisha kuwa yanapatikana haraka.Kamishna wa Sensa, Hajat Amina Mrisho Saidi alisema utoaji wa matokeo ya Sensa kwa mwaka huu ni jambo la kujivunia, akisema hata nchi zilizoendelea matokeo hayo huwa yanachukua muda.
“Tanzania tumeweza kutoa matokeo haya ya awali ndani ya muda wa takriban miezi mitatu tu, kutokana na dhamira ya kweli ya Serikali kufanya Sensa na uzalendo wa wataalamu na wananchi,” alisema.
Alisema ofisi yake itahakikisha kuwa machapisho ya taarifa zote za Sensa, yanatolewa kwa Kiswahili na kusambazwa kwa wananchi ifikapo Juni, mwaka huu.
Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mipango ya Watu, Mary Khan aliipongeza Tanzania kwa kuendesha Sensa na kutoa matokeo ndani ya muda mfupi.
Alisema matokeo ya Sensa hiyo yatawasaidia watunga sera na viongozi ikiwa ni pamoja kufanikisha mipango ya maendeleo na malengo ya kitaifa na kimataifa.
CHANZO-GAZETI LA MWANANCHI

No comments:

Post a Comment