Monday, December 31, 2012

MAANDAMANO YA WANANCHI MTWARA KUPINGA GESI KUSAFIRISHWA DAR YANAFUNUA SERA MBOVU ZINAZOONGOZA NCHI



 Baadhi ya wakazi wa mkoa wa Mtwara Mjini wakiwa kwenye maandamano makubwa waliyoyafanya mapema leo kupinga gesi kusafirishwa kwenda Dar!
 Wakazi hao wakiwa na mabango yao yenye jumbe mbalimbali kama 
 uonavyo pichani
 
Na Joseph Mwambije,Songea
HIVI  majuzi wananchi wa Mkoa wa Mtwara waliandamana kupinga gesi kusafirishwa kupitia bomba kutoka  Mkoa huo kwenda Dares salaam wakitaka vinu vya kuzalisha gesi vijengwe Mtwara ambako wanadai kuna maeneo mengi badala ya Daressalaam.

Habari za maandamano hayo  zilipamba Vyombo vingi vya habari huku zikipewa  uzito mkubwa kwenye  magazeti mbalimbali na kutikisa  Mkoa wa Mtwara na Nchi kwa ujumla na kuzua mjadala mkubwa unaoendelea Nchini.
Maandama no hayo yalikuwa na Lengo moja kubwa kumfikishia Ujumbe Mkuu wa Nchi kwamba  Wanamtwara wanataka kunufaika na rasilimali zao baada ya kunusa harufu ya kutonufaika na rasilimali hizo zinazowazunguka.
Waandamanaji hao ambao walikuwa na Mabango yenye ujumbe mkali  tayari yameshafikisha ujumbe ambao unapaswa kufanyiwa kazi na Kiongozi Mkuu wa Nchi kwa maslahi ya Wananchi wa Mtwara na Nchi kwa ujumla.
Katika Maandamano hayo ambayo yaliwashirikisha wananchi wa wilaya za mkoa huu zikiwamo Tandahimba na Newala, yalianzia katika Kijiji cha Mtawanya hadi Mtwara mjini kupitia barabara ya kwenda Msimbati eneo ambako gesi asilia inapatikana.

Walitembea umbali wa kilomita sita, walitoa maazimio tisa mojawapo likihoji sababu za mitambo ya kuzalisha umeme kutojengwa Mtwara ambako ni jirani na inakochimbwa gesi hiyo.

Katika tamko hilo lenye kurasa mbili, waandamanaji hao wamesema Serikali haijaweka wazi namna gani wakazi wa Mtwara watanufaika na gesi hiyo, huku tayari Rais Jakaya Kikwete akiwa ameshazindua ujenzi wa bomba kwenda Dar es Salaam. Wametaka ujenzi huo usitishwe.

Waandamanaji hao Pia walisema uamuzi wa kupeleka gesi Dar es Salaam unapingana na tamko la Rais Kikwete alilolitoa kwenye ziara yake mkoani hapa mwaka 2009 kwamba ujiandae kuwa ukanda wa viwanda.

Aidha, wanataka vinu vya kuzalishia gesi vijengwe Mtwara kwa kuwa wanayo maeneo ya kutosha ya ujenzi huo tofauti na Dar es Salaam.

“Tunahitaji viwanda vikubwa vijengwe Mtwara ili kuleta ajira kwa wakazi wa Mtwara na mikoa ya jirani, tuna hofu kutokana na ilivyokuwa kwa wakazi wa Songongo (Lindi) kubaki maskini wakati gesi inazalishwa hapo, yasije yakatukuta sisi, hivyo ni lazima tusimamie rasilimali hii ili iweze kuleta maendeleo,” walisema katika azimio lao.

Walibainisha kuwa  Serikali haijaeleza athari zitakazopatikana kutokana na uchimbaji wa gesi katika eneo hilo na namna itakavyoweza kusaidia kuziondoa, huku wakitaka gharama za uunganishaji wa umeme wa nyumbani zisizidi Sh50,000 ili kila mwananchi aone ananufaika na gesi hiyo.

Waandamanaji hao walisema gharama za mradi huo wa kusafirisha gesi hadi Dar sa Salaam ni kubwa, hivyo wakashauri Serikali ichimbe gesi ya Dar es Salaam katika kisima namba 7 ili kuepuka hasara.
Kutokana na maandamano hayo kuna mengi ya kujifunza ambayo Viongozi wetu wanapaswa kujifunza  na kubadili mfumo wa kuendesha Nchi ili unufaishe  sehemu husika pia badala ya kunufaisha Daressalaam pekee.
Hapa kuna tatizo la kimfumo ambalo linapaswa kufanyiwa kazi ili mambo yaende sawa vinginevyo  Wananchi watakuwa wakiandamana kila siku lakini Viongozi wanaweka pamba masikioni wasisikie kile kinacholalalamikiwa na wananchi.
Nasema ni tatizo la kimfumo kwa kuwa maeneo mengi yenye madini yamekuwa hayazinufaishi sehemu husika na tena wananchi wake wamekuwa maskini wa kutupwa huku madini zikienda kujenga sehemuu nyingine.
Kwa mfano katika maeneo mengi yenye madini au miradi mikubwa kodi inalipiwa jijini Daressalaam huku eneo husika lenye madini au mradi husika  linaambulia patupu na kubaki kuunufaisha mji huo muhimu wa kibiashara maana  hiyo ndiyo sifa yake kwa kuwa Mji Mkuu ni Dodoma.
Angalau basi eneo husika ambako madini inapatikana  ingekuwa inapata asilimia fulani kwa maslahi ya wananchi wake na kwa maendeleo ya eneo hilo ili kuondoa migogoro,maandamano na vurugu zinazoweza kuzuilika.
Narudia kusema hili ni tatizo la kimfumo kwa mfano kuna sera moja ya Mamlaka ya mapato Tanzania(TRA)  ya Mlipa kodi anayefikia kulipa kiwango cha kodi kinachofikia milioni 500 kwa mwaka huyu analipia Makao makuu ya Mamlaka hiyo jijini Daressalaam.
Mkoa  unabaki na walipa kodi wadogowadogo  lakini wengine wa kiwango hicho cha milioni 500 wanaratibiwa na Makao makuu na kwa mantiki hiyo basi Wafanyabiashara wakubwa wa kutoka Daressalaam wanaokuja kufanya biashara Mikoani TRA Mikoani haiwezi kushughulika nao sana kwa kuwa wanaratibiwa na Makao Makuu.
Hivyo basi hapa panakuwa na ukwepaji mkubwa wa kodi kwa kuwa wa Mkoani hawezi kushughulika na Mfanyabiashara huyo kwani hawezi kumsaidia katika kufikia lengo la kukusanya kodi kwa mwaka.
Mfanyabiashara huyo inakuwa rahisi kudanganya kwa kuwa anaratibiwa na Makao makuu ambao hawajui biashara zake  mikoni zinakwendaje.
Nayaeleza haya baada ya kuzungumza na Maafisa kadhaa wa TRA ambao walizungumza nami kwa masharti ya kutoandikwa majina yao gazetini.
Katika hili nadhani dhana ya Majimbo inayopigiwa upatu na Chama cha Demokrasia na maendeleo(CHADEMA) ina mantiki kubwa na inapaswa ifanyiwe kazi kwani hata Mataifa makubwa yaliyoendelea kama Marekani yanaitumia vinginevyo tutakuwa tupiga kelee kila siku kulalamikia rasilimali kutonufaisha sehemu husika.
Nitoe mfano  katika Mkoa wa Ruvuma ambako kuna mgodi mkubwa wa Makaa ya mawe ambayo yameanza kuchimbwa na pia madini ya Urani ambayo yako mbioni kuanza kuchimbwa ambayo kama  kodi ingekuwa inakusanya na TRA  Mkoa wa Ruvuma basi Mkoa huo ungepaa katika ukusanyaji wa mapato.
Basi angalau asilimia Fulani ingeingia katika makusanyo ya kodi ya Mkoa ili kuupaisha Mkoa kimapato badala ya kila kitu kuwa Daressalaam na kufanya hata Wabunge wetu washinde huko baada ya kuupata Ubunge kwa kuwa pesa zetu zinakimbizwa huko.
Nimelizungumza hili kwa kuwa linashabihiana na na lile la Mtwara ambako Wananchi waliandamana kupinga gesi kusafirishwa kwenda Daressalaam.Tunapaswa kubadili mifumo inayoendesha Nchi na Sera zake vinginevyo tutabaki kulia kila siku huku machozi yetu yakienda na maji kama samaki.
Mwisho.
Mwandishi wa  Makala hii ni Mchambuzi wa masuala ya kisiasa kijamii na Kimataifa.
Anapatikana kwa-0755 761195
                              0655761195
mwambije.blogspot.com 

 

 Waandamanaji wakiwa wamekusanyika kwenye moja ya uwanja mjni Mtwara mapema leo wakipinga gesi kusafirishwa kwenda jijini Dar! 

No comments:

Post a Comment